Mwaka mmoja baada ya tetemeko kubwa la ardhi lililoikumba Morocco, jamii za milimani ambazo ziliathiriwa zaidi bado zinajenga upya.
Katika mji wa Amizmiz, ulioko katika eneo lililoathiriwa sana la Al Haous, baadhi ya majengo yamefanyiwa ukarabati, lakini mengi yamesalia katika hali ya ubovu kama siku ya tetemeko la ardhi.
Abderrahim Alachoun, fundi bomba kutoka Amizmiz, anaonyesha matumaini kwa siku zijazo huku akikiri kwamba baadhi ya wakazi bado wanasubiri usaidizi. “Tunamshukuru Mungu kumekuwa na maboresho; hatari imepungua. Pia tunahitaji kubadilisha mtazamo wetu kutoka zamani wakati hakuna mtu aliyekuwa akifanya kazi na tulikabiliana na matatizo. Hivi sasa, hali zinaendelea kuimarika polepole. Baadhi ya wakazi wamepata msaada [wa kiserikali] huku wengine bado wanasubiri.”
Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 6.8, ambalo lilikuwa na nguvu zaidi kuwahi kutokea Afrika Kaskazini katika kipindi cha miaka 120, lilitokea Septemba 8, 2023, na kuua karibu watu 3,000.
Majengo mengi katika vijiji na miji inayozunguka Milima ya Juu ya Atlasi ya Morocco, ikiwa ni pamoja na Amizmiz, yameharibiwa na kuwa magofu.
Katikati ya vifusi vilivyoondolewa kwa uangalifu, baadhi ya majengo bado yamesimama, huku mengine yakiwa yametelekezwa au kuharibiwa.
Njia ya kurudi kwenye hali ya kawaida imeanza, ingawa inaendelea polepole.
Rakouche Ait Rouh, mkazi wa Amizmiz, alisema: “Nilipokea mipango kutoka kwa mamlaka mwezi Februari. Vifusi viliondolewa mwezi Juni. Sasa, kwa bahati nzuri, nimeanza mchakato wa kujenga upya nyumba yangu.”
Katika mwaka uliopita, wakaazi wamelazimika kupitia urasimu tata kupata pesa zinazohitajika kujenga upya nyumba zao.
Baada ya kutathmini uharibifu huo, mamlaka ilitenga kati ya euro 8,000 na 16,000 ($8,900 hadi $17,800) kwa kaya kwa ajili ya ujenzi upya, zilizogawanywa katika malipo kadhaa.
Baadhi ya kaya pia zilipata usaidizi wa haraka wa kifedha.
Wale ambao hawakupata msaada walilazimika kutafuta vyanzo vingine vya fedha ili kujenga upya au kubaki kwenye makazi ya muda huku wakisubiri taratibu muhimu za kuanza ujenzi kukamilika.
Ingawa matetemeko ya ardhi ni nadra katika Afrika Kaskazini, tukio la mwaka jana lilikuwa moja ya nguvu zaidi kuwahi kurekodiwa katika eneo hilo.